Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu
(Nyaumata Mkoani)

Sherehe ya amani na upendo na uchapakazi

Posted on: July 10th, 2020

Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu imefanya sherehe fupi ambayo imewakutanisha  viongozi mbalimbali ndani ya Mkoa na wafanyakazi wa Hospitali ya Rufaa ya Simiyu tarehe 10 Julai, 2020 katika ukumbi wa Bariadi Conference Hall


Mgeni rasmi katika sherehe hiyo alikuwa ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Simiyu, Bi Mariam Perla Mmbaga.Bi Mariam, aupongeza uongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu kwa kufanya jambo lenye manufaa,  kuburudisha na kujenga moyo na molali  wa kufanya kazi kwa watumishi wote. Pia mgeni rasmi alifurahishwa sana  na utaratibu unaofanywa na Hospitali katika kuwapatia mafunzo (Induction Course) waajiriwa wapya pindi wanaporipoti katika kituo cha kazi ambayo yanafungua fursa na uwajibikaji katika Utumishi wa umma wa wafanyakazi hao.

Kwa upande mwingine Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu, Dkt Matoke Muyenjwa alifurahishwa sana na mwitikio chanya wa viongozi na watumishi wengine katika kufanikisha  sherehe hiyo.

Aidha Dkt Matoke  alisisitiza kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi,kutoa huduma bila upendeleo na pia aliwaasa wafanyakazi kuendelea kudumisha upendo, mshikamano na umoja kwa kuzingatia sheria, kanuni,taratibu na maadili katika utumishi wa Umma.

Katika kunogesha sherehe hiyo wafayakazi wa Hospitali ya Rufaa ya Simiyu walitoa zawadi kwa Mganga Mfawidhi, Dkt Muyenjwa ikiwa ni ishara ya upendo na mshikamano kwa kiongozi huyo.

Sherehe hiyo ilitanguliwa na michezo mbalimbali ya mbio za miguu, kukimbiza baiskeli kwa upande wa wanamke na wanaume na kumalizika kwa mtenange wa mpira wa mguu kati ya uongozi wa Hospitali (HMT) na wafanyakazi toka idara na vitengo mbalimbali ndani ya Hospitali